Wednesday, June 16, 2010


Imefahamika kuwa majambazi mawili yaliyouawa na polisi mwishoni mwa wiki iliyopita jijini Arusha saa 5.40 asubuhi katika eneo la Unga LTD walikuwa wakivizia kupora fedha zinazodaiwa kuwa ni mishahara iliyokuwa ikitolewa benki.

Akielezea tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Basilio Matei alisema kuwa jeshi la polisi lilipata taarifa za siri kuwa majambazi hao walipanga kupora mishahara ambayo hata hivyo hakuweka wazi ilikuwa ikipelekwa kwenye kampuni ipi.


Alisema kuwa jeshi hilo liliandaa mpango wa siri na kugundua gari walilokodisha ambalo ni Toyota Corolla na kuwafuata nyuma kwa gari binafsi na walipofika katika Barabara iendayo eneo la Faya majambazi hao waligundua kuwa wanafuatiliwa.

“Mara baada ya kubaini kuwa wanaowafuatilia ni askari walijihami kwakufyatua risasi hewani na ndipo polisi walipojibu shambulizi hilo na kuwafyatulia risasi ambapo wawili waliuawa,” alisema Kamanda Matei.

Kamanda Matei aliwataja waliouawa kuwa ni Erick Massawe (35), Mkazi wa Kijenge na Michael Raphael (36), Mkazi wa eneo la Sanawari na kwamba jeshi hilo bado linamtafuta mmoja aliyekimbia .


Utata unajitokeza kuhusu mauaji hayo kwani inadaiwa majambazi hao waliuawa wakiwa ndani ya gari ambalo linahusishwa na jeshi la polisi na kuwepo kwa tundu moja ya risasi ambalo linaonekana ni risasi iliyongia ndani ya gari na siyo kutoka.

Pia dereva wa gari walilokuwepo watu hao waliotajwa kuwa ni majambazi hafahamiki alipo na wajihi wake .

Wananchi walioshuhudia tukio hilo wamedai kuwa, hakukuwa na majibishano ya risasi kati ya polisi na majambazi hayo.


“Jeshi la polisi linahitaji kujipanga zaidi na pengine hata kujisafisha kufuatia baadhi ya askari wake kuhusishwa na uhalifu wa kushiriki ujambazi,” alisema mwananchi mmoja aliyeomba jina lake kuhifadhiwa.

Matei pia amebainisha kuwa polisi jijini Dar es Salaam inawashikilia majambazi wanaodaiwa kuhusika na mauaji ya mfanyabiashara wa Kiarabu, Salehe Hussen Ally ,ambapo mbali na mauaji, yalifanikiwa kupora mamilioni ya shilingi katika duka la la Burj Al Arab lililopo katikati ya mji wa Arusha. Majambazi hayo yataletwa jijini Arusha.

Majambazi watetemesha Arusha!!

Na Woinde Shizza
wa Michuzi Blog (Globu ya Jamii), Arusha

Kundi la majambazi watatu wakiwa na silaha nzito limeua watu wawili akiwemo mfanyabiashara mwenye asili kiasia na kupora mamilioni ya fedha mijni hapa.

Tukio hilo ambalo limethibitishwa na polisi mkoani hapa limetokea jana majira ya saa kumi na nusu jioni katika mtaa wenye shughuli nyingi za kibiashara wa Sonali Soko Kuu mjini Arusha.

Watu walioshuhudia tukio hilo wamesema kuwa kabla ya mauaji hayo majambazi, ambayo idadi yake yake kamili haijaweza kufahamika, yaliteka mtaa huo na kupiga risasi hovyo hewani na kusababisha taharuki katika eneo hilo na maeneo ya jirani.

Katika tukio hilo mfanyabiashara Swaleh Hussein Alli (35) aliuawa kwa kupigwa riasi kadhaa kichwani na kufariki dunia papo hapo, huku mfanyabiashara ndogo ndogo mwanamama Paschalina Antony (32) mkazi wa Unga Limited aliuawa kwa kupigwa risasi kifuani wakati akipiga mayowe bada ya kushuhudia majambazi hayo yakammiminia risasi Alli.

Mashuhuda hao walisema kuwa kabla ya tukio hilo walifika watu kadhaa na kuingia katika duka la mfanyabiashara huyo wakijifanya wanataka kufanya manunuzi. Ghafla tu watu hao kila mmoja akiwa na silaha walimnyooshea bunduki mfanyabaishara huyo na kuwaamuru wafanyakazi wa duka hilo kulala chini na kuanza kumiminia risasi mfanyabaishara huyo.

“Tukio lenyewe lilikuwa kama filamu hivi watu hao waliingia dukani kama wateja wakauliza bei ya nguo na vitu vingine wakati tunajaribu kuwaonyesha ghafla wakageuka na kukaa kila upande na silaha wakatuamuru kulala,tulichiosikia ni milio ya risasi na harufu ya damu tulipoamka tukamkuta tajiri yetu amekufa”alisema mmoja wa watumishi wa duka hilo ambaye hakutaka kutajwa jina gazetini.

Naye John Kumbau mfanyabiashara wa soko kuu alisema kuwa majambazi hayo yalikuwa mengi na yalipofika katika eneo hilo yalijigawa katika makundi matatu na kuhakikisha kuwa hayana mtu wa kuwazuia baada ya tukio.

“Unajua mimi niliona kila kitu kwa hofu ya kuuawa nikanyamaza kimya,yule mama aliyeawa alipiga kelele nikaona akipigwa nikakaa kimya lilikuwa tukio la kutisha”alisema Kumbau

Akizungumzia tukio hilo kamanda wa jeshi la polisi mkoani hapa Basilo Matei alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuongeza kuwa majambazi hayo yalikuwa na gari aina Toyota Corrola Premio lenye rangi ya kijivu ambapo mapaka sasa namba zake za usajili hazijaweza kufahamika.

Kamanda Matei alibainisha kuwa uchunguzi wa awali unaoonyesha gari hilo liliporwa kutoka mjini Moshi siku tatu kabala ya tukio hilo .

“Baada ya tukio hilo tulifanya mawasilianio ya haraka na majirani zetu ,tukajulishwa kuwa gari hilo lililotumika liliporwa kutoka Kilimanjaro”alisema Matei.

Aidha aliwataka wananchi mkoani hapa kutoa taarifa zozote zitakazoasaidia kukamatwa kwa wahusika wa tukio hilo baya kuwahi kutokea katika siku za hivi karibuni.

“Wahusika wa tukio hili lazima watakamatwa hawataweza kuuushinda mkono mrefu wa dola kila mahali tumejizatiti ni lazima watiwe nguvuni.

Tukio hilo kubwa la mauaji na uporaji ndilo tukio kubwa kuwahi kutokea mwaka huu baada ya watu wanaoasadikiwa majambazi kumwua mwanamke mmoja aliyetajwa kwa jina Jackline Deo mkazi wa Lemara mwishoni mwa mawezi januari mwaka huu ambapo hata hivyo katika tukio hilo majambazi hayo hayakuchukua kitu chochote na baada ya siku tatu nao waliuawa na polisi.

Sakata la "Kikwete" na "Mimba za Vihelehele" laombewa msamaha


Shikamoni watanzania wote. Watoto msisite kuitikia salamu yangu ambayo ndani yake ina unafiki wa kuonesha jinsi gani nilivyomuungwana kwa watu wote.
Moyoni nataka kutimiza lengo langu la kisiasa la kumuombea msamaha Rais wangu Jakaya Kikwete kuhusu kauli aliyoitoa Kijijini Kisesa wilayani Magu mkoani Mwanza, kwamba kukithiri kwa mimba mashuleni kunachochewa na viherehere vya wanafunzi wenyewe.

Kwa haki ya Mungu aliye juu, nachukua nafasi hii, kumuombea radhi kwa Watanzania wote Rais Kikwete kwa sababu ni mmoja kati ya ndugu zangu, yaani nimekuwa rafiki wa familia ya marehemu dada yake aliyekuwa anakaa mtaa wa Mtoni pale Temeke, jirani na eneo la Sokota, nazungumzia jijini Dar es Salaam.
Mkiniona chozi langu namaanisha nina tikiswa kumtima na haka ka kauli ka ndugu yangu, ambako kamewafanya Wanyamwezi wenzangu, licha ya vitabia vyao vya kupenda ‘totozi’ wakutane kimila kujadili kama ni kweli watoto wao wanabeba mimba kwa viherehere vyao au ni hali isiyovumilika inawaondolea uvumilivu watoto na kujikuta watake wasitake wanalazimika kufanya ngono.

Mzee Maganga, kikao chenu kina maana sana na ni kweli mtakuwa mmekasirika, lakini mnashindwa kufahamu kuwa kama ninyi msivyobahatika kuingia Ikulu, na Rais naye hajapata bahati ya kujionea maisha ya watoto wenu na shida mnazokutana nazo.
Aliposema hivyo alikuwa hajui kama watoto wenu wa kike wanakata misitu minene kabla ya kuifikia shule yenu ya sekondari ya kata mliyojenga kwa lazima ya yule kiongozi shujaa aliyeng’atuka kwa kale ka tuhuma ka umeme.
Kati yenu ni nani aliyemwambia Rais Kikwete kwamba kuna baadhi ya wanafunzi mmewapangisha kwenye nyumba za nyasi zilizopo kijiji jirani na shule na kwamba huko wanajihudumia kwa kila kitu?

Mlimwambia Rais kwamba ninyi wazazi hamna uwezo wa kuwapatia hata thumni ya chumvi watoto wenu kwa vile mmekatazwa kuuza mazao yenu nje ya nchi na tena mmekopwa mazao na vyama vya ushirika ambavyo vinatarajia kuwalipa kidogo kidogo mwishoni mwa mwaka huu?
Unaona sasa! Wote mnatikisa vichwa kuonesha hamjamwambia! Hii ina maana kwamba rais hajui maisha yenu, yeye kazoea kuwaona watoto wa mjini wakienda shule kwa magari na shilingi mia mbili mfukoni. Kwa mazingira hayo atakuwa na kosa kweli kutamka kuwa watoto wenu wanaviherehere vya mabwana? Aaa, jamani mbona mnataka kumfanyia tambiko kwa kumuonea mtoto wa mwenzenu, kumbukeni ni mtani wenu huyo!

Kama nilivyosema mwanzo, naandika uchochezi huu kumuombea radhi mkuu wangu, nikikiri kwamba kidogo sana, narudia tena, kidogo alikosea kusema hivyo na kilichomkosesha baada ya mimi kumsoma nilipokuwa naye kichwani kwa uchambuzi wa suala hili la mimba kwa wanafunzi ni kudanganywa na wasaidizi wake.
Kinachotokea siku hizi, wengi wao wanaogopa kutimuliwa kazi, hivyo huwa hawataki kueleza ukweli, mtakumbuka hata janga la njaa lilipotokea kijijini kwenu mkuu wenu wa wilaya alidiriki kusema kwamba hamna njaa na kwamba stoo zenu zilikuwa na chakula cha kutosha.

Sasa tusikimbilie huko nafahamu kwamba walikufa akina Mataluma, Mwana Ushi na watoto wa mzee Mikidadi wawili katika njaa hiyo, huo ulikuwa ni mfano tu wa namna viongozi wa juu wanavyoweza kutoa taarifa za uongo kwa lengo la kulinda posho zao. Msibubujikwe na machozi wazee, Rais hakuwa na nia ya kuwakejeli watoto wenu alikosea kutokana na ‘data’ ndiyo maana alisahau hata kama kondomu hazifiki kwenu na kwamba hata zikifika hamna uwezo wa kununua.

Mzee Kapaga bado hamjanielewa? Nadhani sasa naanza kuona mkono wa kisiasa ndani ya kauli hii, maana kama ni kosa la mimba za viherehere mbona nimeshalifafanua sana, au mnataka niwageukie na ninyi kuhusu uharibifu wa mila mlioufanya mpaka watoto wenu wamekuwa hawaheshimu usichana wao.
Hata kama utandawazi umeharibu tabia za watoto wenu ni jukumu lenu kama wazazi kuwakataza wanenu waache

Tuesday, June 15, 2010

Hii ni kali kuliko! Hebu isome.

Mwalimu afundisha shule nzima yeye peke yake! Duh!

Mkuu wa Sekondari Kibungo Juu, Tarafa ya Matombo, Bw. Chapembe Chapembe, ndiye mwalimu pekee anayefundisha wanafunzi 270 kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne na amelazimika kutoifunga shule hiyo kwa likizo iliyoanza Juni mwaka huu.

Uamuzi wa kuendelea kufundisha madenti hao wakati wa likizo ni kwa ajili ya kuwawezesha madenti wa kidato cha nne na pili ambao wanatarajia kufanya mitihani yao mwaka huu wamudu vyema kufaulu masomo yao.

Mwalimu Mkuu huyo alisema hayo juzi mjini Morogoro katika hafla ya kumkabidhi pikipiki kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mh. Issa Machibya, baada ya kutambua ushupavu wake wa kujituma katika kufundisha kwenye mazingira magumu, uwajibikaji na kuipenda kazi yake.

Kwa mujibu wa Mwl. Chapembe, shule hiyo ilianza mwaka 2007, na kati ya wanafunzi hao 114, wasichana ni 81, mwaka huu ilipangiwa wanafunzi 79 wa kidato cha kwanza na inatarajia kutoa wanafunzi zaidi ya 53 wa kwanza wa kidato cha nne.

Alisema shule hiyo iliyopo katika uwanda wa milima na miinuko, inakabiliwa na changamoto za kukosa walimu na nyumba za kuishi, hali iliyomfanya kubaki peke yake na mwaka huu wanafunzi wake watafanya mitihani ya kumaliza sekondari.

“Walimu wote wanaopangiwa Kibungo Juu hufika na kuondoka kutokana na mazingira magumu … usafiri ni wa shida na nyumba hakuna,“ alisema Mkuu wa Shule.

Aliongeza: “Mimi mwenyewe ninaishi Kijiji cha Kiswira ni umbali wa zaidi ya kilometa 40 kutoka ilipo shule, na mara nyingi nalazimika kupiga kambi shuleni ili kuwafundisha vizuri wanafunzi wangu,” alisema.

Mkuu huyo alisema amelazimika kuwatumia wanafunzi wa kidato cha nne wa Sekondari ya Tawa kufundisha wenzao wanaotarajia kufanya mitihani mwaka huu kwa baadhi ya masomo.

Wanafunzi wa shule hiyo wengi wao wana uwezo mkubwa kiakili, lakini wanachokosa ni nyongeza ya maarifa na mbinu za kitaaluma kutoka kwa walimu wenye taaluma ya masomo ya sekondari.

“Bado ninawahurumia wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne kama watamudu kufanya mtihani kikamilifu … ninaona ipo hatari ya wanafunzi kushindwa mitihani yao ya mwaka huu,” alisema Chapembe.