Friday, May 25, 2012

RAIS WA MPITO WA MALI YUPO SALAMA



Rais wa Mpito wa Mali, Dioncounda Traore.


Waandamanaji wakiwa Ikulu baada ya kuvamia. Picha na Reuters
WAKUU wa serikali nchini Mali wamesema kuwa Rais wa Mpito, Dioncounda Traore, amepelekwa eneo salama baada ya kupigwa hadi kuzirai na mamia ya waandamanaji nchini humo.
Mamia ya waandamanaji walimshambulia Rais Traoure wakipinga mkataba ulioafikiwa na Tume ya kiuchumi ya nchi za magharibi mwa Afrika, ECOWAS, ambapo Traoure ataendelea kutawala hadi mwaka mmoja badala ya siku 40 pekee zilizokubaliwa miezi miwili iliyopita.
Mwandishi wa BBC amesema kuwa shambulio hilo limewashtua wanadiplomasia waliokuwa wakifanya kila juhudi kurejesha amani na utangamano nchini humo.
Muda wa kuongoza aliopewa kiongozi huyo, Djouncounda Traore ulitarajiwa kukamilika Jumatatu.
Lakini viongozi wa nchi za Magharibi mwa Afrika, waliafikia mkataba na kiongozi wa mapinduzi Kapteni Amadou Sanogo kwamba Bw. Traore asalie mamlakani ili aweze kuongoza harakati za uchaguzi na kumaliza harakati za waasi wa Tuareg.
Mkataba huo pia ulijumuisha mpango wa kukubalia Sanogo atajwe kama kiongozi wa zamani alipwe mshahara wa rais na apewe nyumba ya kifahari.
Mapinduzi hayo pamoja na harakati za waasi kuteka Kaskazini mwa Mali, yamesababisha maelfu ya watu kutoroka makwao.
Mashirika ya misaada yanasema wana wasiwasi mkubwa kuhusu hali ya kibinadamu nchini Mali nchi ambayo pia inakumbwa na baa la njaa.
Mwandishi wa BBC mjini Bamako, Martin Vogl amesema kuwa wanajeshi waliwaruhusu baadhi ya waandamanji kuingia katika ikulu ya rais ingawa bwana Traore hakuwepo wakati huo.
CHANZO: BBC SWAHILI

No comments: