Saturday, June 30, 2012

RIPOTI KAMILI KUHUSU DK. ULIMBOKA

Na Waandishi Wetu
NYUMA ya kipigo alichopewa kiongozi wa madaktari ambao wako kwenye mgomo nchi nzima, Dk. Steven Ulimboka kuna siri nzito, Ijumaa lina ripoti kamili.
Gazeti hili lilinyetishiwa mkanda mzima na mtu aliyekuwa na Dk. Ulimboka (jina tunalo ambaye naye ni daktari) usiku wa kuamkia Jumatano wiki hii kwenye Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni jijini Dar es Salaam.

MUVI LA MATESO LAANZA
Jamaa huyo alidai kuwa, wakiwa viwanjani hapo wakipooza koo, walifika watu watano waliojitambulisha kuwa ni askari wakiwa na silaha ambapo walidai kuwa walimfuata Dk. Ulimboka na kumwambia anatakiwa Kituo cha Polisi Kati (Central).
Ilidaiwa kuwa Dk. Ulimboka alishurutishwa kupanda kwenye gari leusi ambalo halikuwa na namba za usajili na kuondoka eneo hilo huku akiacha gumzo kuwa Central anapelekwa kwa ishu gani.
Ikadaiwa kuwa baada ya Dk. Ulimboka kuchukuliwa, marafiki zake walitoka spidi kuelekea Central kujua kulikoni na pia kumwekea dhamana.
Jamaa huyo alidai kuwa marafiki zake walipofika Central hawakumkuta na wala hakukuwa na dalili za Dk. Ulimboka kufikishwa mahali hapo.
Aliendelea kudai kuwa walianza kufanya mawasiliano usiku huo ili kujua rafiki yao alipelekwa wapi lakini jitihada hizo hazikuzaa matunda.

SIMU HAIPATIKANI
Alidai wakiwa Central, askari mmoja aliwataka kutulia hadi asubuhi wangepata taarifa kamili kwani kwa wakati huo hata simu yake ilikuwa haipatikani.
Jamaa huyo alidai kuwa saa 12:00 asubuhi alipokea simu kutoka kwa msamaria mwema aliyekuwa maeneo ya Mabwepande nje kidogo ya Jiji la Dar akamwambia kuna mtu amemkuta akiwa taabani ambaye alimtajia namba kwa shida ili aipige na kutoa taarifa ya hali yake.
“Alisema alimtajia namba tu na hakumsesha tena,” alisema rafiki huyo wa Dk. Ulimboka.
Alidai kuwa baada ya kujulishwa habari hiyo alitaka aende mwenyewe lakini alipoomba ushauri watu walimsihi asiende peke yake.
Jamaa huyo alisema alitafuta watu akaenda nao na walipofika huko walimkuta Dk. Ulimboka aliyechukuliwa akiwa mzima hajitambui na hakuwa na uwezo wa kuzungumza.
Alisema kuwa baada ya kumuona mwenzao alivyochakazwa, wakamchukua na kumpeleka kwenye Kituo cha Polisi cha Bunju ambapo yule msamaria mwema alitoa maelezo jinsi alivyomkuta.
Rafiki huyo wa Dk. Ulimboka alidai kuwa, katika maelezo ya yule msamaria mwema alisema kuwa alishtuka alipomkuta akiwa porini na hali mbaya huku akiwa amefungwa kitambaa cheusi usoni na kutapakaa madonda mabichi mwili mzima.
Baada ya kuchukuliwa maelezo walipatiwa PF-3 ambapo walifanya jitihada za kumkimbiza katika Hospitali ya Muhimbili kwa kutumia ambulance ya AAR, alipofikishwa tu madaktari wenzake walianza kumpa matibabu ya hali ya juu ili kunusuru uhai wake huku mgomo wao ukiendelea.

MTU ALA KIPIGO
Wakati anafikishwa Muhimbili tayari wanaharakati mbalimbali walishajitokeza ili kumpokea lakini mara baada ya kufikisha mtu mmoja aliyesadikiwa kuwa ‘njagu’ aliingia chooni na akasikika akizungumza na simu.
Ilidaiwa kuwa katika mazungumzo yake alisikika akisema kumbe jamaa hajafa, jambo lililoibua hisia kwamba alijua kilichoendelea.
Ilisemekana kuwa watu waliomsikia wakamchomoa na kumpa kipigo cha mbwa mwizi hadi Radio Call inayotumiwa na polisi ikamchomoka kwenye suruali kabla ya askari waliokuwa doria kumwokoa na kuondoka naye.

KOVA ATHIBITISHA
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alithibitisha kutokea kwa tukio hilo linalodaiwa kuwa la utekaji na kuongeza kuwa uchunguzi unafanyika na sheria itachukua mkondo wake dhidi ya wahusika.

Wananchi waishauri serikali
Wakiongea na Ijumaa mara baada ya tukio hilo kutokea, baadhi ya wananchi wameitaka serikali kuhakikisha uchunguzi wa kina na wa haraka unafanyika na ripoti yake kuwekwa hadharani ili kuondoa utata uliotawala.

Imeandaliwa na Haruni Sanchawa, Issa Mnally na Makongoro Oging.
Dk Ulimboka akiendelea kupata matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kitengo cha mifupa (MOI) kwenye chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).

No comments: