Monday, November 19, 2012

TGNP YAVIPONGEZA VYOMBO VYA HABARI

Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Profesa Ruth Meena akijibu maswali ya wahariri mbalimbali katika mkutano wa TGNP na wahariri hao uliofanyika jana jijini Dar es Salaam, pembeni yake ni Kaimu Mkurugenzi wa TGNP, Mary Nsemwa.
Mmoja wa wahariri kutoka vyombo vya habari vinavyomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), Jane Mihanji  na Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) akichangia mada katika mkutano wa TGNP na wahariri wa habari.
Mhariri kutoka Global Publishers, Walusanga Ndaki (wa kwanza kulia) akiwa na baadhi ya wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa katika mkutano huo.
Mwandishi wa habari na mmiliki wa Francis Godwin Blog  akiwa katika mkutano huo.
Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TGNP, Profesa Ruth Meena (kulia) pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa TGNP, Mary Nsemwa.
Mmoja wa maofisa wa TGNP kutoka Idara ya Habari na Mawasiliano, Deo Temba (kushoto) akichukua kumbukumbu katika mkutano huo na wahariri. Pembeni yake ni Prof. Ruth Meena.
Na Mwandishi wa Thehabari.com
KAIMU Mkurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Mary Nsemwa amevipongeza vyombo mbalimbali vya habari nchini kwa kile sasa kutoa nafasi ya kuridhisha kwa kuandika masuala mbalimbali ya kijinsia ambayo hapo awali yalikuwa hayapewi nafasi ya kutosha.
Bi. Nsemwa ametoa kauli hiyo leo jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na wahariri mbalimbali wa vyombo vya habari katika mkutano wao na TGNP, kuzungumzia changamoto anuai za kijinsia na vyombo vya habari pamoja na ushiriki wa wanawake katika mchakato wa maoni ya uundwaji wa katiba mpya.
Alisema ushirikiano mzuri uliojengeka kati ya taasisi hiyo na vyombo vya habari umesaidia kwa kiasi kikubwa hivyo masuala ya kijinsia na hasa yale yanaowakandamiza wanawake kusikika katika vyombo vya habari hali ambayo imesaidia kwa kiasi fulani.
“…Tumejifunza mengi kutoka katika vyombo vya habari, vyombo hivi sasa vimewaunganisha wanawake…sauti za wasiosikisa hasa wa vijijini sasa zinasikika kupitia vyombo hivi. Vyombo vya habari pia vimepaza sauti kwa kampeni yetu ya Haki ya Uchumi; ‘Rasilimali Ziwanufaishe Wanawake walioko Pembezoni’ na mkumbuke kwamba nyinyi mnanguvu zaidi yetu,” alisema Bi. Nsemwa.
Naye mmoja wa Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Profesa Ruth Meena akiwasilisha mada katika mkutano huo wa wahariri alisema mambo mengi ya msingi ambayo ni miongoni mwa madai ya wananchi yameainishwa katika Katiba iliyopo sasa, hivyo kushauri ipo haja ya kuangalia namna ya usimamizi wa sheria na mabadiliko kadhaa kuingizwa kwenye Katiba Mpya.
“...Kwa upande mmoja  Katiba Ya Jamhuri Ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inatoa haki sawa kwa wanawake na wanaume katika nyanja za siasa, uchumi na ustawi wa jamii, na hapohapo  kuzipokonya kwa mkono mwingine kwa kuruhusu kuendelezwa kwa sheria, taratibu na tabia zinazokinzana na katiba,” alisema Prof. Meena.
Aidha alishauri Katiba mpya ibatilishe sheria zote zinazokinzana na haki za msingi za wanawake na watoto wa kike hususani kubatilisha sheria na mila zote za ubaguzi wa jinsia, ubaguzi dhidi ya watoto hususani watoto wa kike, katika maswala ya ndoa, mirathi, haki za kumiliki.
“Kwa mantiki hii, katiba ibainishe kwa uwazi haki za wanawake na haki za watoto. Pamoja na kuwajibisha serikali kuchukua hatua zote za kisera na sheria ili kulinda na kuhifadhi haki za wanawake na za watoto katika maeneo hayo, na pia iwajibishe serikali kutekeleza mikataba yote iliyoridhia kuhusu haki za wanawake ( CEDAW, CRC, ILO Conventon) Mikataba hii itambulike kuwa ni sheria za nchi  ili kuepusha ucheleweshaji wa kutafsri au kuruhusu uchakachuaji wamikataba hii katika sheria za nchi,” alifafanua Prof. Meena.
Pamoja na hayo alishauri Katiba mpya iangalie haki ya ufikiaji wa huduma za jamii; haki ya kufikia na kufaidi  huduma za msingi kama vile maji, chakula, malazi na elimu na hifadhi ya jamii ziendelee kuwepo - pamoja na kusisitiza wajibu wa serikali wa kuhakikisha huduma hizi za msingi zifikiwe  na ke na me ( rika zote, na hali zote).

No comments: