Thursday, August 1, 2013

WAKATI SHEIKH PONDA AKITANGAZA KUGOMBEA URAIS, POLISI YATANGAZA KUMKAMATA KWA KUFANYA MIHADAHARA YA UCHOCHEZI


CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) visiwani Zanzibar kimemtuhumu Mwenyekiti wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda, kuwa anaendesha kampeni za uchochezi wa kidini.


Uchochezi huo umedaiwa kuhatarisha amani ya nchi, hivyo kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama kumchukulia hatua za kisheria.


Katibu wa Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu (NEC) Zanzibar, Itikadi na Uenezi, Waride Bakari Jabu, alisema jana kuwa ni wiki moja sasa tangu Ponda afanye mihadhara kwenye misikiti ya Mbuyuni, Kwarara na Nungwi kisiwani Unguja.


Waride alisema kuwa hotuba za Sheikh Ponda alizozitoa kwa nyakati tofauti kwenye misikiti hiyo zinapandikiza mbegu ya chuki, kuondosha upendo na kuhatarisha amani.


Alisema matamshi yake ni hatarishi kwa amani na utulivu uliopo, kwani anawataka Waislamu kupigana vita ya dini (Jihad) na kushiriki harakati za kuikomboa Zanzibar, kwa madai kuwa serikali iliyoko madarakani inawakandamiza na kuwanyanyasa wananchi.


“Sheikh Ponda ni hatari, anapanda shari na chuki miongoni mwa wananchi, anahamasisha wananchi wafanye uasi, kulipiza visiasi na kutaka waingie barabarani kwa maanadano ya kutetea haki kama inavyotokea Misri,” alisema.


Aidha, alisema CCM imeshangazwa na ukimya wa vyombo vya ulinzi na usalama wa raia kumtazama kiongozi huyo bila ya kumchukulia hatua za kisheria wakati akiwatukana matusi ya nguoni viongozi wa serikali na chama tawala.


Aliongeza kuwa Sheikh Ponda huenda anatumiwa na mtandao wa vurugu ili kuharibu na kuvuruga amani ambapo hamu yake ni kuona damu ya wananchi ikimwagika na nchi ikiingia kwenye machafuko.


Kwa mujibu wa Waride, kitendo cha Ponda kulitumia jukwaa la dini na kufanya siasa misikitini hakikubaliki na kwamba kikiachiwa kiendelee kinaweza kuleta madhara na mgawanyiko.


Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mussa Ali Mussa, alisema jeshi hilo limeanza kumtafuta Sheikh Ponda tangu walipopokea taarifa za kuendesha mihadhara ya uchochezi katika baadhi ya misikiti, ikiwa na lengo la kuibua chuki.


Mussa alisema kitendo anachokifanya kinakwenda kinyume cha sheria, hivyo kumtaka popote alipo ajisalimishe kwa hiari yake.


Tangu kuingia visiwani Zanzibar, Sheikh Ponda amekuwa akifungamana na viongozi wa Jumuiya ya Uamsho wakipinga kitendo cha viongozi wa jumuiya hiyo kuendelea kubakia mahabusu baada ya kukamatwa na kufunguliwa mashtaka ya uharibifu wa mali na kuhatarisha usalama wa taifa.


Viongozi hao wa Uamsho wako mahabusu baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka Zanzibar, Ibrahim Mzee Ibrahim, kuwasilisha ombi la kufunga dhamana yao kwa kutumia sheria ya Usalama wa Taifa na marekebisho yake ya mwaka 2002

Tanzania Daima

No comments: