Monday, August 6, 2012

YANGA WAMUWASILISHA MWALI WA KAGAME BUNGENI LEO


MABINGWA WA NCHI 12 AFRIKA; Yanga na Kombe la Kagame baada ya kuifunga Azam 2-0
Na Mahmoud Zubeiry, Dodoma
MABINGWA wa soka Afrika Mashariki na Kati, Yanga SC ya Dar es Salaam leo wanatarajiwa kutambulisha Kombe la ubingwa wa michuano hiyo, maarufu kama Kombe la Kagame katika ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mini Dodoma.
Yanga, waliotwaa Kombe hilo mara mbili mfululizo sasa, wachezaji wake waliwasili usiku wa jana na baadhi ya viongozi, Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, Titus Osoro, Mohamed Bhinda na George Manyama pamoja na Katibu Mkuu, Celestine Mwesigwa na Meneja, Hafidh Suleiman, wakati Mwenyekiti, Yussuf Manji na Makamu wake, Clement Sanga na Wajumbe wengine watawasili mapema leo.
Kwa upande wa timu, wachezaji walifika pia jana na makocha wasaidizi, Freddy Felix Minziro na Mfaume Athumani Samatta, wakati kocha Mkuu, Mbelgiji Tom Saintfiet atakuja leo pamoja na viongozi wakuu.
Mbali na Manji, Sanga na kocha, katika msafara unaokuja leo wanatarajiwa kuwamo, Wajumbe wa Baraza la Wadhamini, Francis Mponjoli Kifukwe na Mama Fatuma Karume.
Yanga ilitwaa Kombe la Kagame kwa mara ya pili mfululizo wiki iliyopita, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kuifunga Azam FC mabao 2-0, ambayo yalitiwa kimiani na Hamisi Kiiza ‘Diego Milito’ na Said Bahanuzi ‘Spider Man’.
Hiyo kwa ujumla ilikuwa mara ya tano mfululizo, Yanga inatwaa Kombe hilo, baada ya awali kuchukua mwaka jana, wakiifunga Simba katika fainali bao 1-0, Uwanja wa Taifa mfungaji Kenneth Asamoah ambaye ametemwa, ingawa siku hiyo Kiiza pia alifunga bao safi, ambalo refa alilikataa.
Yanga ilichukua kwa mara ya kwanza Kombe hilo, mwaka 1975 ikiifunga tena Simba katika fainali, mabao 2-0 wafungaji Sunday Manara ‘Computer’ na Gibson Sembuli (sasa marehemu) Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Ikachukua tena mwaka 1993, Uwanja wa Nakivubo, Kampala, Uganda kwa kuifunga SC Villa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na Said Nassor Mwamba ‘Kizota’ (sasa marehemu) na Edibily Jonas Lunyamila.
Ilichukua tena mwaka 1999, ikiifunga tena SC Villa, Uwanja wa Nakivubo, kwa penalti 5-3, kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 120, Yanga ikisawazisha bao kupitia kwa Lunyamila, baada ya Hassan Mubiru kutangulia kuifungia Villa, siku hiyo Manyika Peter akicheza penalti mbili za Waganda.

No comments: